Mashairi Bomba.
SHAIRI: KUMBE NI……
MTUNZI: FAM
Sikuwa na wasiwasi, katika yangu safari, naeleza
Sikutaka mfuwasi, wala sikupanda gari, sikiliza
Sikupenda kujighasi, sikuifanya kikiri, sikuweza
Nilikwenda polepole
Njia nikaiandama, sio ya barabarani, nawambia
Popote sikusimama, japo yekuwa mwituni, mwasikia
Khofu kwangu ikahama, hatembea kwa amani, sehofia
Sikuogopa chochote
Kwa mbali nikasikia, sauti iliyo kali, inanita
Huku kwato zanijia, zimekazana kwa kweli, sikusita
Na wala sikukimbia, nikenda bila kujali, kwatakwata
Njia nikaiandama
Nilipofika kwa mbele, wallahi sikuamini, sikioni
Nesikia makelele, yasema Mimi ni jini, maluuni,
Metumwa nije nikule, kafara ya kijijini, huamini?
Moyo ukaanza khofu
Nyuma nilipogeuka, roho yekwenda mbinguni, mara moja
Neona bonge la joka, linavichwa sabiini, linakuja
Vizuri likanishika, likanitia kinywani, halengoja
Ghafula nikashituka
(Mpemba Orijinali)